Friday, February 3, 2017

Polisi yarushiwa lawama ucheleweshaji kesi



Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) mkoani Shinyanga,  kilisema polisi na uhaba wa mahakimu ni vyanzo vya ucheleweshaji wa upatikanaji haki. Kaimu Mwenyekiti wa TLS mkoani hapa, Paul Kaunda alisema polisi wanaohusika na upelelezi wamekuwa wakitumia muda mrefu bila sababu ya msingi.

Pia, alisema polisi wanaotumiwa na Jamhuri kama mashahidi  wamekuwa hawahudhurii wanapohitajika  kutoa ushahidi.

Wakati hayo yakijiri mkoani Shinyanga, Hakimu Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Bukombe, Gabriel Kulwijila alisema mashauui mengi ya makosa ya jinai hucheleweshwa na polisi wanaotumia muda mrefu kufanya uchunguzi.

Hakimu Kulwijila aliomba polisi kukamilisha upelelezi kwa wakati na kukusanya ushahidi mahusus kwa weledi, utakaosaidia mahakama kutenda haki.

Licha ya polisi kudaiwa kuchelewesha kesi, ilidaiwa kuwa  mikoa ya Kagera na Mara inaongoza kwa vishoka wasiokuwa na ujuzi wa fani ya sheria, hali inayochangia kuchelewesha utoaji haki. Mwenyekiti wa TLS Mkoa wa Kagera, Wakili Aaron Kabunga alisema vishoka wamefungua ofisi na kwamba wanatoa ushauri wa kupotosha wananchi.

“Mkoa wa Kagera unaongoza  kuwa na vishoka ukifuatiwa na Mara, tunaitaka Serikali ichukue hatua kwani wanashiriki upotoshaji ambao husababisha wananchi kupoteze haki zao mahakamani,’’ alisema Kabunga.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Bukoba, Seif Kulita alisema wanaoruhusiwa kusaidia wananchi ni wanasheria waliotimiza masharti, lakini siyo vishoka.

Mkoani Mwanza, Mahakama Kuu mwaka jana ilipokea mashauri 4,994 kati ya hayo 2,216 tayari yametolewa uamuzi.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, Robart Makaramba alisema kati ya hayo, mashauri 2,879 yalibaki mwaka 2015, huku mengine 2,115 yalipokewa mwaka jana.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella alisema mkoa huo unakabiliwa na migogoro ya ardhi kwa kiwango kikubwa, hivyo jitihada zikilenga kutoa haki pekee bila kutatua migogoro hiyo zinaweza zisifanikiwe.


No comments:

Post a Comment

New Posts

Libya yatangaza hali ya dharura ya mwaka mzima baada ya mafuriko

  Serikali ya Libya imetangaza hali ya dharura ya mwaka mzima kwa shabaha ya kuzuia kuenea magonjwa ya kuambukiza katika maeneo yaliyokuumbw...