Friday, April 14, 2017

Obby Claud Blog Tunakutakia Heri ya PASAKA


Bwana Yesu Asifiwe!
Tunamshukuru Mungu Baba kwa kutupa neema hii ya kushirikishana Neno la Mungu kwa Njia hii tena. Kesho tutakuwa tukiadhimisha sikukuu ya Pasaka, na makanisa mengi hivi sasa yapo kwenye majira ya kiibada ya Pasaka. Na Mungu ashukuriwe kwa kutupa neema ya kuadhimisha Pasaka katika mwaka huu wa 2012.
Wewe kama mwana wa Mungu, hupaswi tuu kuadhimisha Pasaka kwa mazoea, bali inakupasa na ni vyema sana kuadhimisha Pasaka kuanzia moyoni mwako, kwani Mungu anawatafuta watu watakaomwabudu katika roho na kweli.( Yohana 4:23 ), hivyo basi, napenda kwa msaada wa Roho Mtakatifu, tuyatafakari mambo machache kuhusu siku kuu hii ya Pasaka.
HISTORIA YA PASAKA
Katika Biblia, Pasaka ilianza kwa mara ya kwanza katika kitabu cha Kutoka 12, tafadhali tenga muda ukisome kitabu hiki kizima. Katika Pasaka hii ya kwanza, wana wa Israel waliagizwa kupakaa damu ya kondoo kwenye vizingiti vya juu na miimo ya milango yao kabla ya Mungu kuleta pigo la kumi kwa watu wa Misri, ambalo lilikuwa ni pigo la kuwauwa wazaliwa wote wa kwanza wa Wamisri.
Mungu aliagiza WaIsrael wapakae damu hiyo kwenye milango yao ili Malaika atakapokuwa anapita kuwaua wamisri, asiwaue na WaIsraeli pia. Na Malaika alipokuwa akipita, aliwaua wazaliwa wa kwanza wa Wamisri, na aliacha kudhuru kila nyumba ya WaIsraeli, mradi tuu iwe imepakwa damu ya kondoo mlangoni.


DAWA ILIKUWA YA LAZIMA
Katika Kutoka 12:23, inasema “ BWANA apitapo katika nchi yote kuwapiga Wamisri, ataiona damu kwenye vizingiti na kwenye miimo ya milango naye atapita juu, wala hatamruhusu mwangamizi kuingia katika nyumba zetu na kuwapiga ninyi “. Jambo lililotakiwa hapa ili na Waisraeli wasipigwe, na wao kuweka damu kwenye milango yao. Bwana alichokuwa anaangalia si kuona kama nyumba fulani ni ya Muisrael au la, Yeye alikuwa anaangalia kama kuna damu mlangoni au la. Hii ina maana kuwa kama Mwisrael yeyote asingepakaa damu ya kondoo huyo katika mlango wake, angeangamia pamoja na Wamisri. Umeona msisitizo wa damu katika Pasaka hii ya kwanza? Na siku hiyo ndiyo siku ambayo wazaliwa wa kwanza wa Wamisri walikufa, na Waisraeli wote wakatoka utumwani Misri na kuanza safari ya kuelekea katika nchi ya Kaanani waliyoandaliwa na Bwana.
Na baada ya hayo, Mungu aliwaagiza WaIsrael kuiadhimisha siku hii daima na hata akasema “Watoto wenu watakapowauliza, ‘Sikukuu hii ina maana gani kwenu?’,Basi waambieni, ‘Hii ni dhabihu ya Pasaka kwa BWANA, ambaye alipita juu ya nyumba zetu alipowapiga Wamisri“( Kutoka 12:26-27 ). Kwa hiyo kuadhimisha Pasaka ni agizo la Mungu. Na pia Mungu akaendelea kusema “ Kwa sababu BWANA aliutenga usiku ule ili kuwatoa Waisraeli katika nchi ya Misri katika usiku huu Waisrael wote wanapaswa kuadhimisha kwa kukesha ili kumheshimu BWANA katika vizazi vijavyo. ” (Kutoka 12:42 ).
Hivyo ndivyo namna Pasaka ilivyoanza kwa agizo la Mungu mwenyewe, na ukisoma katika Kutoka 12, ndivyo ilivyoendelea kuadhimishwa mara nyingi katika kipindi cha Agano la Kale. Kuna wakati wana wa Israel walikaa muda mrefu sana bila kuadhimisha Pasaka, lakini kila mara alipoinuka mtu aliyeisoma sheria ya Mungu, walitubu na kuendelea tena kuadhimisha siku hii ya Pasaka.
Kwa siku ya leo nimeona nikukumbushe namna Pasaka ilivyoanza ili usiwe unaadhimisha Pasaka kwa namna ya mwili tu, bali uadhimishe Pasaka kuanzia moyoni. Na ikitokea umeulizwa na mtu asiyeamini au asiyefahamu, basi uwe tayari kumweleza kwa upole kuhusu Pasaka. Nitakuletea sehemu ya pili ya somo hili ili kujifunza zaidi pia.


New Posts

Libya yatangaza hali ya dharura ya mwaka mzima baada ya mafuriko

  Serikali ya Libya imetangaza hali ya dharura ya mwaka mzima kwa shabaha ya kuzuia kuenea magonjwa ya kuambukiza katika maeneo yaliyokuumbw...