Friday, January 6, 2017

Majambazi yajeruhi watatu kwa risasi, yapora fedha, simu

KAMANDA WA POLISI MKOA WA KIGOMA, FERDINAND MTUI.

Majeruhi wote watatu wamelazwa katika Hospitali ya Mkoa Maweni kwa matibabu.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kigoma, Ferdinand Mtui, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo.

Kamanda Mtui alisema watu wawili ambao hakuwataja majina yao, wametiwa mbaroni na upelelezi unaendelea ili sheria ichukue mkondo wake.

Baadhi ya watu walioshuhudia tukio hilo, walidai kuwa majambazi hao wawili walikuwa na bunduki moja aina ya Sub Machine Gun (SMG) na mapanga.

Waliojeruhiwa katika tukio hilo wametambuliwa kuwa ni Hussein Ndoroma (30), Hamad Bwanajoro (36) na Sifa Salum (40), wote wakazi wa Gungu.

Mmoja wa majeruhi ambaye ni mmiliki wa duka hilo la huduma za fedha kwa mtandao wa simu aliyelazwa wodi namba saba hospitalini hapo, Ndoroma (30), alisema tukio hilo lilitokea juzi saa 2:00 usiku akiwa katika sehemu yake hiyo ya biashara.

Ndoroma alisema akiwa hapo dukani kwake, aliingia mmoja wa majambazi hao akiwa na panga na kumuamuru akae chini na ampe fedha.

"Nilikataa kutii amri hiyo na kuanza kupambana naye na nilipomzidi nguvu, jambazi huyo aliomba msaada kwa mwenzake ambaye alikuwa nje na bunduki aina ya SMG akanifyatulia risasi paja langu la mguu wa kulia na ikatokea mguu wa kushoto.

Nilianguka chini nakupoteza fahamu na aliposhtuka nilijikuta nipo hapa hospitalini," alisema Ndoromo.

Alisema alipoanguka chini, majambazi hayo yalipata fursa ya kupora simu tano na fedha taslimu Sh. 200,000 na kutokomea kusikojulikana.

Kwa mujibu wa Ndoromo, moja kati simu zilizoporwa na majambazi hayo, ilikuwa na salio la Sh. 700,000.

Ndoromo ameliomba Jeshi la Polisi mkoani humu kuweka askari wa doria maeneo ya Gungu hasa nyakati za usiku kwani kumekuwapo na matukio ya ujambazi mara kwa mara.

Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Mkoa Maweni, Fadhili Kibaya, alithibitisha kupokea majeruhi watatu wa risasi ambao wanaendelea kutibiwa hapo.

Kibaya alisema kati ya majeruhi hao, wawili ni wanaume na mmoja ni mwanamke na hali zao zinaendelea vizuri.

No comments:

Post a Comment

New Posts

Libya yatangaza hali ya dharura ya mwaka mzima baada ya mafuriko

  Serikali ya Libya imetangaza hali ya dharura ya mwaka mzima kwa shabaha ya kuzuia kuenea magonjwa ya kuambukiza katika maeneo yaliyokuumbw...